Chuji: ‘Katika maisha yangu ya soka, sijawahi kukutana na mtu kama Bonny


Kiungo wa zamani wa Yanga na timu ya taifa ya Tanzania ‘Taifa Stars’ Athumani Idd ‘Chuji’ amesema wazi kuwa, katika maisha yake ya soka hajawahi kucheza na mtu mwenye kiwango kikubwa kama Geoffrey Bonny licha ya kucheza na wachezaji wengi mahiri.

“Katika maisha yangu ya mpira sijawahi kukutana na mtu wa aina ya Bonny, nimekutana na watu wengi lakini yeye tulikuwa tunaenda sawa akicheza chini mimi nicheze juu au mimi nicheze chini yeye juu,” – Chuji.

Chuji na Bonny walicheza pamoja wakiwa Yanga pamoja na timu ya taifa ya Tanzania, hapa Chuji akaitaja mechi ambayo walicheza kwa kiwango cha juu akiwa na Bonny katika safu ya kiungo.

“Nimecheza mechi nyingi na Bonny na zote kwa pamoja tulicheza vizuri sana, lakini kuna mechi ya kimataifa Stars tulicheza na Cameroon hapa nyumbani, yeye alicheza chini mimi nikacheza juu tulifanya mambo makubwa baada ya kutoka uwanjani kila mtu akawa anamwambia mwenzie kazi uliyofanya leo si mchezo.”

Chuji amesema kikubwa ni kumuomba Mungu aweze kuilaza roho ya marehemu mahala pema peponi na sote tupo njia moja licha ya mweznzetu kutangulia.

No comments